Na Beatrice Moses, Mwananchi
Dar es Salaam. Kamati ya Bunge
ya Hesabu za Serikali, PAC, imepanga kuzikutanisha kwa pamoja, Wizara za
Fedha na Elimu wakati ikipokea taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa
Hesabu za Serikali (CAG) inayohusu matumizi ya fedha za marejesho ya
rada jinsi zilivyotumiwa.
Akizungumza Dar es Salaam jana, Makamu Mwenyekiti
wa kamati hiyo, Deo Filikunjombe alisema kuwa wanatarajia kupokea
taarifa hiyo kesho na watatumia fursa hiyo kujihakikishia kama matumizi
hayo yalikuwapo au kama kulikuwa na ulaghai wa aina yoyote.
“Kwa sasa ni mapema kuanza kufikiri kwamba fedha
hazikutumika inavyotakiwa, lakini kama kuna ujanja wowote ulifanyika
tutabaini tu alisema na kuongeza:
“Ndiyo sababu katika kikao hiki tunakutana wote;
CAG, Wizara ya Fedha na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi ili kama
kuna maswali basi kuwe na majibu yake papo hapo,” alisema Filikunjombe.
Alisema leo watapokea taarifa ya ukaguzi maalumu
kuhusu mbolea ya ruzuku, pia shughuli nyingine ambazo kamati inatarajia
kuzifanya katika kipindi cha wiki mbili zijazo ni pamoja na kutembelea
bandari na kukagua mradi wa kuzalisha umeme kwa kutumia makaa ya mawe
wilayani Ludewa.
Awali mwaka jana aliyekuwa Naibu Waziri wa Fedha,
Janeth Mbene, aliliambia Bunge kwamba fedha za rada zilizorejeshwa
Sh72.3 bilioni ziliingizwa katika bajeti ya serikali kwa mwaka 2012/13.
Mbene alisema kwamba fedha hizo ni marejesho kwa
Serikali ya Muungano kutokana na udanganyifu uliofanywa na Kampuni ya
BAE Systems ya Uingereza wakati wa kuiuzia Serikali ya Tanzania rada ya
kuongozea vyombo vya usafiri angani.
Fedha zilizorudishwa na kampuni hiyo baada ya
Taasisi ya Uchunguzi wa Makosa Makubwa ya Jinai (SFO) ya Uingereza
kubaini kuwa, baadhi ya maofisa wa Serikali ya Tanzania na mawakala wa
ununuzi kupandisha bei baada ya kushawishiwa na kampuni hiyo.
Novemba mwaka jana Serikali ilianza kusambaza
vitabu milioni 19.4 kwa shule za msingi nchini, ambavyo ilielezwa kuwa
vimenunuliwa kwa chenji ya rada na asilimia 75 ya fedha hizo zimetumika
kununulia vitabu hivyo na asilimia 25 zitatumika kununulia madawati.
MWANANCHI
MWANANCHI
No comments:
Post a Comment