Mbeya. Taifa Stars inahitaji kusafisha nyota leo
mbele ya mashabiki wa soka mkoani Mbeya na Tanzania kwa ujumla kwa
kuitandika Malawi ‘The Flame’ katika mchezo wa kimataifa wa kirafiki
utakaochezwa kwenye Uwanja wa Sokoine jijini hapa.
Wapenzi wa soka mkoani Mbeya walianza jana
kupeperusha bendera ya Taifa kila kona huku gari la matangazo
likizunguka mitaani kuwahimiza wajitokeze kwa wingi kujionea mchezo huo
kwa kiingilio cha Sh5,000.
Hata hivyo, mchezo huo unatarajiwa kuwa mkali
kutokana na ukweli kwamba timu zote zitataka kufuta machozi ya kufungwa
katika mechi za kirafiki zilizochezwa wiki mbili zilizopita, ambapo
Stars ilinyukwa mabao 3-1 na Burundi wakati Flame ilitandikwa 4-1 na
Zimbabwe, ambao wana mchezo na Stars mwishoni mwa mwezi huu.
Kocha msaidizi wa Malawi, Jack Chamangwana alisema
timu yake itacheza kwa nguvu zote ili kupata kipimo cha mwisho kabla ya
kuikabili timu ya Taifa ya Chad jijini Lilongwe, wiki chache zijazo
katika moja ya mechi za kuwania kufuzu kwa michuano ya Mataifa ya
Afrika.
Naye kocha mpya wa Stars raia wa Uholanzi, Martinus Nooij alisema kwa kifupi wamejiandaa kuikabili Malawi kikamilifu.
Nooij alisema timu yake iliyoweka kambi mjini
Tukuyu, wilayani Rungwe mkoani hapa inaendelea vizuri na ilifika juzi
jijini Mbeya kufanya mazoezi kwenye Uwanja wa Sokoine ili kuuzoea.SOURCE>>MWANANCHI
No comments:
Post a Comment