Shigongo akizungumza kwa masikitiko jinsi watu wengi walivyo kwenye hatari ya kufa kwa ugonjwa wa ini.
KAMPENI ya ugonjwa wa Homa ya Ini unaosambazwa na Virusi vya
Hepatitis B inazinduliwa rasmi leo, Machi 7, mwaka huu katika Hospitali
ya Mkoa wa Kitabibu Ilala – Amana, jijini Dar es Salaam. Akizungumza na
Ijumaa, Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Global Publishers ambayo ndiyo
inayoendesha kampeni hiyo, Eric Shigongo alisema, kama kampuni
wameguswa na ugonjwa huo hivyo wamedhamiria kupambana kwa nguvu zote
kuuzuia.“Homa ya Ini ni ugonjwa hatari sana, maana ukimpata mtu kinachofuata ni kifo. Naweza kusema ni ugonjwa hatari zaidi kuliko hata Ukimwi, lakini tofauti yake na Ukimwi ni moja; huu una kinga. “Ni lazima tuungane kama taifa, huu ugonjwa ni hatari sana, sisi Global Publishers tumeanza, kinachofaa ni wewe na yule kujitokeza ili tuishinde hii vita pamoja. Leo tunaizindua rasmi,” alisema Shigongo na kuongeza: “Ndugu zetu wengi sana wanapoteza maisha kila siku kutokana na ugonjwa huu wa Homa ya Ini, lakini kwa sababu chanjo ipo, lazima tuchukue hatua.
Sisi Global Publishers tumeamua kuchukua jukumu la kuhakikisha Hepatitis B unatokomezwa.” Kampeni hii inaendeshwa na Global Publishers kwa kushirikiana na Hospitali ya Amana, Megra Clinic, Sanofi Pasteur, Damu Salama na SD Africa.
No comments:
Post a Comment