EBENEZA MARCH 9 2014

EBENEZA MARCH 9 2014

Tuesday, August 12, 2014

LIVERPOOL YAMTAKA ETO'O.

KLABU ya Liverpool inafanya majadiliano ya kutaka kumchukua Samuel Eto’o katika kipindi hiki ambacho wanahitaji kusajili mshambuliaji. Eto’o kwasasa yuko huru baada ya kuachwa na Chelsea mwishoni mwa msimu uliopita na anaweza kuongeza uzoefu katika kikosi cha Liverpool kinachonolewa na Brandan Rodgers. Rodgers amekuwa akitafuta mshambuliaji toka dili na Loic Remy lilipokwama na Eto’o anaweza kuchagua lao sahihi. Uzoefu wa nyota huyo mwenye umri wa miaka 33 hususani mataji matatu aliyoshinda ya Ligi ya Mabingwa Ulaya unaweza kumsaidia kwasababu Liverpool imerejea katika michuano hiyo baada ya miaka mitano na hawana wachezaji wa kutosha wenye uzoefu nayo. Mbali na Liverpool kuonyesha nia na Eto’o, Inter Milan na Ajax Amsterdam nazo pia zimezungumza na wawakilishi wa mchezaji huyo.
CABALLERO ATAMBA KUCHUKUA NAMBA YA JOE HART, CITY.
GOLIKIPA mpya Willy Caballero ana hamu kubwa ya kuchukua nafasi ya Joe Hart kama golikipa namba moja wa Manchester City msimu huu. Kipa huyo wa kimataifa wa Argentina alisajiliwa akitokea Malaga Julai ambapo alicheza katika mechi yake ya kwanza ya kimashindano akiwa na mabingwa hao wa Ligi Kuu wakati walipotandikwa mabao 3-0 na Arsenal katika mchezo wa Ngao ya Jamii. Caballero amesema anatamani kuendelea kubakia katika nafasi hiyo wakati kikosi cha City kinachonolewa na Manuel Pellegrini kitakapoanza kutetea taji lake katika mchezo dhidi ya Newcastle United Agosti 17 mwaka huu. Kipa huyo alikiri kuwa anataka kuwa namba moja wakati akihojiwa na atafanya mazoezi kwa bidii ili kuhakikisha anamshawishi kocha wake kumpa nafasi ya kuanza.
CHAMA CHA SOKA ITALIA CHAPATA RAIS MPYA.
CHAMA cha Soka nchini Italia kimepata rais mpya Carlo Tavecchio aliyetangazwa jana. Tavecchio mwenye umri wa miaka 71 alikuwa makamu wa rais wa shirikisho hilo toka mwaka 2009 lakini alithibitisha kugombea kugombea nafasi hiyo kufuatia uamuzi wa Giancarlo Abete kuamua kujiuzulu baada ya Italia kutolewa mapema katika michuano ya Kombe la Dunia iliyofanyika Brazil Juni mwaka huu. Pamoja na kampeni zilizojaa utata huku akituhumiwa kwa masuala mbalimbali Tavecchio alipambana na kuhakikisha anamshinda mpinzani wake ambaye ni nyota wa zamani wa AC Milan Demetrio Albetini na kuteuliwa kuwa rais mpya wa FIGC. Kibarua cha kwanza cha Tavecchio kitakuwa ni kusaidia kutafutwa kwa kocha mpya wa timu ya taifa ya nchi hiyo huku kocha wa zamani wa Juventus Antonio Conte akipewa nafasi kubwa ya kuchukua nafasi hiyo.
GFA YAUNDA KAMATI KUIIMARISHA BLACK STARS.
CHAMA cha Soka nchini Ghana-GFA kimeunda kamati ya watu watatu itakayokuwa na jukumu la kuteua mshauri wa ufundi katika kikosi cha timu ya taifa ya nchi hiyo, Black Stars. Hata hivyo maofisa wa GFA wamesisitiza kuwa mshauri wa ufundi atakayeteuliwa atakuwa na jukumu la kusimamia mfumo mzima wa Stars na sio kocha pekee. Umuazi wa kuteua kamati hiyo kwa mujibu wa taarifa ya GFA umepelekwa katika kikao cha kamati ya utendaji ya chama hicho kufuatia kupitia muelekeo wa ufundi wa kikosi cha timu ya taifa. Kamati hiyo ya watu watatu itaongozwa na makamu wa rais wa GFA Fred Crentsil ambaye atafanya kazi sambamba na Fred Pappoe na Francis Oti Akenteng. Taarifa ya GFA iliendelea kudai kuwa kamati hiyo itafanya pamoja na kocha wa Black Stars Kwesi Appiah ili kutafuta mtu atakayeweza kuipeleka timu ya taifa katika muelekeo unaofaa.
ANCELOTTI AWASHUSHUA WANAOMTAKA KHEDIRA, ADAI HANA MPANGO WA KUMUUZA.
MENEJA wa klabu ya Real Madrid, Carlo Ancelotti amevionya vilabu vya Arsenal na Chelsea kumuacha Sami Khedira kwani kiungo huyo hauzwi. Nyota huyo wa kimataifa wa Ujerumani amekuwa akihusishwa kuondoka Santiago Bernabeu toka waliposhinda Kombe la Dunia mwezi jana huku Uingereza pakitajwa kama kama uelekeo wake. Usajili wa Mjerumani mwenzake Toni Kroos kutoka Bayern Munich ndio ulionekana kuchangia kwa kiasi kikubwa nyota huyo kuhusishwa na kuondoka lakini Ancelotti amekanusha tetesi hizo na kudai kuwa Khedira bado ana mkataba nao unaomalizika kiangazi mwakani hivyo bado atabakia klabu hapo kwa kipindi hiki. Madrid wanahatarisha kumkosa Khedira bila kupata chochote kama wakishindwa kumshawishi asaini mkataba mpya wa mabingwa hao wa Ulaya wakati wa msimu 2014-2015.

No comments:

Post a Comment