SHIRIKA la Umeme Tanzania (Tanesco),
limeanzisha operesheni maalumu ya kukusanya madeni yanayofikia Sh
bilioni 233, ambapo wateja watakaokaidi zikiwamo taasisi za umma na
binafsi, zitakatiwa umeme. Akizungumza na waandishi wa habari Dar es
Salaam jana, Mkurugenzi Mkuu wa Tanesco, Felchesmi Mramba alisema kati
ya fedha hizo, Sh bilioni 129 ni za taasisi za Serikali ikiwamo Zanzibar
inayodaiwa Sh bilioni 70 na Sh bilioni 104 watu, taasisi binafsi na
viwanda.
“Kwa sasa shirika limeanzisha kampeni
maalumu ya kukusanya madeni itakayojumuisha kutoa notisi ya kutaka
wateja kulipa ndani ya muda huo na kuwakatia wote ambao hawajalipa.
“Tunawataka wateja wote walipe madeni yao mapema iwezekanavyo ili kuepuka usumbufu,” alisema.
Kukatika umeme Mramba pia alikiri
kutokea kwa hali ya kukatika umeme katika baadhi ya maeneo ya nchi hasa
Kanda ya Ziwa na baadhi ya maeneo ya Dar es Salaam hasa Ubungo na
katikati ya Jiji hivi karibuni.
Akielezea hali hiyo, alisema
ilisababishwa na hitilafu za mtambo zilizotokea katika vituo vya Sokoine
na Ubungo, Dar es Salaam pamoja na kuanguka kwa nguzo kubwa mbili za
vyuma wilayani Kahama.
Alifafanua, kuwa Ubungo kulitokea wizi
wa nyaya za shaba za ambazo inaaminika wezi hao huziuza kama chuma
chakavu. Kwa upande wa Kahama, kulitokea wizi wa vyuma ambavyo wezi
huvitumia kutengeneza mikokoteni ya kukokotwa na ng’ombe na majembe ya
kulimia ya plau.
“Tumepata hasara kubwa ya Sh bilioni 1.2
Kahama na Sh milioni 200 Ubungo. Tunatoa rai kwa Watanzania kujali
miundombinu ambayo ni rasilimali ya Taifa na kuepuka vitendo vinavyoleta
usumbufu kwa Watanzania wenzao, kusababisha hasara na kurudisha nyuma
hatua kubwa za maendeleo zilizokwishapigwa,” alisema.
Umeme wa mafuta Kuhusu hali ya
uzalishaji umeme, Mramba alisema ni ya kuridhisha na hakuna upungufu wa
umeme pamoja na mahitaji ya huduma hiyo kuendelea kuongezeka.
Hata hivyo, alibainisha kuwa bado
Tanesco inaendelea kutumia mitambo ya mafuta ya kuzalisha umeme wa
dharura ambao ni ghali, ili kukidhi ongezeko la mahitaji linaloendelea.
Mahitaji ya umeme kwa sasa kwa mujibu wa Mramba ni megawati 898 tofauti
na ilivyokuwa mwaka jana, ambapo mahitaji yalikuwa megawati 851.
“Hii imelazimu kuzalisha umeme zaidi ili
kukidhi mahitaji haya ya ziada. Ni muhimu kufahamu kuwa kiasi kikubwa
cha uzalishaji kinatokana na mitambo ya mafuta,” alisema.
Alielezea uwiano wa mchango wa mitambo
hiyo katika kukidhi mahitaji, kwamba mitambo ya mafuta, ambayo ndiyo
ghali zaidi, inatoa asilimia 45 ya umeme unaozalishwa.
Mitambo ya gesi ambayo ni ghali pia
lakini si kama ya mafuta, inatoa asilimia 42 ya umeme huo, huku mitambo
ya maji ambayo ndiyo inayotoa umeme kwa gharama nafuu zaidi, ikichangia
asilimia 13 tu ya mahitaji ya umeme nchini.
Rekodi ya wateja Katika hatua nyingine,
Tanesco imevunja rekodi ya kuunganishia umeme wateja 143,000 mwaka jana,
idadi ambayo haijawahi kufikiwa tangu kuanzishwa kwa shirikia hilo.
Hata hivyo, Mramba alisema bado kuna
maombi mengi hayajafanyiwa kazi, lakini akaahidi kuwa wateja wote
walioomba kuunganishiwa umeme mwaka jana, watahudumiwa kwa kasi na
ifikapo Februari wataanza kupata huduma hiyo.
“Tutaendelea kuwaunganishia umeme kwa
kasi kama tulivyoahidi ili ifikapo mwishoni mwa Februari tuwe
tumewaunganishia. Vifaa vinaendelea kuwasili na kazi zinaendelea
vizuri,” alisema Mramba. Ili kuendeleza kasi hiyo, alisema Tanesco
itabadilisha utaratibu wa ununuzi wa vifaa ili kuondokana na matatizo ya
mara kwa mara ya uhaba.
“Hii itajumuisha ununuzi wa vifaa kwa
wingi mikoani ili kupunguza mlundikano wa majukumu yanayofanyika makao
makuu,” alisema. Hujuma mitandaoni Mramba pia alielezea masikitiko yake
kutokana na kuibuka kwa baadhi ya watu wanaohujumu shirika hilo katika
mitandao ya mawasiliano nchini.
Kwa mujibu wa Mramba kuna akaunti za
mtandao wa twitter zilizoanzishwa na baadhi ya watu zinazodaiwa
kuanzishwa na Tanesco. “Twitter hizi zimekuwa zikitumika kuchafua
shirika na kukejeli wateja.
Majina yake ni Tanesco@TANESCO-, TanescoEscobar@tanescobar na TANESCO LTD-@tanesco-,” alisema.
Alisema wameiharifu Mamlaka ya
MawasilianoTanzania (TCRA) na Jeshi la Polisi, ili wachukue hatua
stahiki kwa mitandao ya kijamii inayotumika kulichafua shirika hili kwa
kufungua akaunti kwa kutumia jina la Tanesco.
SOURCE: HABARI LEO
No comments:
Post a Comment