VYAMA
vikubwa viwili hasimu hapa nchini, Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Chama
cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) vimeingia katika ‘vita’ mpya.
Wakati CCM
ikituhumiwa kutumia dola na msajili wa vyama vya siasa ‘kukishikisha’
adabu CHADEMA, likiwamo tamko zito la kutaka kukifuta kwa madai ya
kuhatarisha amani nchini, chama hicho pinzani kimeapa kupambana na
yeyote kwa gharama zozote dhidi ya kile walichokiita dhuluma, uonevu na
ukandamizaji wa haki za binadamu kunakofanywa na serikali.
Akihutubia
kwa mara ya kwanza tangu kuachiwa kwa dhamana makao makuu ya polisi na
kunusurika kwa bomu katika mkutano wa kufunga kampeni jijini Arusha hivi
karibuni, Mwenyekiti wa taifa wa CHADEMA, Freeman Mbowe, alisema sasa
chama hicho kitaongeza kasi ya mapambano bila kumwogopa yeyote.
“Sitamuogopa rais, lakini nitamheshimu, sitaogopa polisi lakini nitawaheshimu, sitaogopa Jeshi lakini nitaheshimu Jeshi.
“Kuanzia
sasa sitamheshimu mtu yeyote asiyeheshimu ubinadamu wa mtu mwingine.
Uchaguzi wa juzi wa kata, tumeshinda kwa mapambano ya damu. Watu wetu
wamepigwa kila mahali, wamekatwa mapanga na mashoka na vijana wa CCM,
Green Guard.
“Katika hali
kama hiyo siwezi kucheka na polisi, ndiyo maana juzi tumetangaza
kuwapatia vijana wetu mafunzo ya ukakamavu ili tujilinde na vitendo
hivi. Hatujaanzisha jeshi, tulichokisema na kukisimamia ni hiki.
“Wananchi wa
Songea, huu ni mkutano wangu wa kwanza kuhutubia hadharani tangu
nilipokoswa koswa kuuawa kwa bomu, risasi za SMG na risasi za bastola
kwenye tukio la Soweto, Arusha siku ya kuhitimisha kampeni.
“Lakini
napenda niwaambie kitu kimoja, miye kama kamanda wenu mkuu, sitaingiwa
hofu. Sasa tuna usongo zaidi na wametuongeza charge (nguvu) ya kuing’oa
CCM katika chaguzi zijazo, maana tunajua tunasimamia haki, ukweli na
matumaini ya Watanzania wote,” alisema.
Huku
akiwatoa machozi baadhi ya waliohudhuria mkutano huo wa juzi, baada ya
kuona kitabu kimojawapo chenye picha za watu waliouawa na kuteswa na
vijana wa Green Guard ya CCM, Mbowe aliuita ushindi wa kata nne za
jijini Arusha kuwa ni wa damu zilizomwagika za wanachama wake.
“Kama kuna
mtu alifikiri kuwa kumuua au kutaka kumuua Mbowe atamtia hofu...huyo mtu
ameshindwa. Kwa kweli siku ile mimi na wengine tuliokuwa walengwa
kabisa wa lile tukio tulinusurika kwa mipango ya Mungu tu. Ni kwa sababu
tunaongozwa na Mwenyezi Mungu, tutaendelea kupigania haki hadi
kieleweke.
“Huko
Serengeti, kwenye Kata ya Machila, watu wetu wake kwa waume wametekwa
nyara, wakapelekwa na kufichwa kwenye nyumba ya CCM, wengine wamebakwa,
wengine wamewekewa chupa sehemu za siri, kwa sababu tu ya CHADEMA,”
alisema.
Mbowe alidai
kuwa amesikitishwa na upotoshaji mkubwa unaofanywa kwa makusudi na CCM
na serikali kwamba chama chake kimeanzisha jeshi, kiasi cha kuvisukuma
vyombo vya dola kuanza kuwakamata viongozi wa juu wa chama hicho.
“Hatuwezi
wala hatuna mpango wa kuanzisha jeshi kama ambavyo polisi wanataka
kupotosha kwa kusoma habari zinazoandikwa na magazeti ya CCM na
kutangazwa na TBC.
“Nani hajui
kuwa CCM wana kikundi kinaitwa Green Guard ambacho kiko nchi nzima,
kinapiga wananchi, kinaumiza wapinzani na ushahidi tunao wa kutosha,
kinapewa mafunzo ya kijeshi na ushahidi tunao.
“CHADEMA
tumeshalalamika na kulia mara chungu nzima kuwa si sahihi vitendo hivi
kuendelezwa, hakuna anayetusikiliza, si polisi wala si serikali. Wote
wamekaa kimya. Wakati mwingine vitendo hivi vinafanywa mbele ya
usimamizi au macho ya polisi, kila siku wanaoumizwa ni CHADEMA. Sasa
tukasema basi, kuendelea kulialia ni uendawazimu,” alisema.
Mbowe
alisema walichokiamua ni kufanya ulinzi shirikishi au ulinzi jamii kama
ambavyo polisi wamekuwa wakiasa na kusihi kila siku.
“Tulichokisema
wala si kitu kipya kabisa. Kimo ndani ya katiba yetu. Naomba mtu yeyote
hapa anayeweza kusoma apande hapa juu asome hii katiba ya chama hapa,
inazungumzia Red Brigade. Tunachofanya sasa hivi ni kuwapatia vijana
ukakamavu. Hatuanzishi jeshi, wala hatutakuwa na mabomu, wala bunduki,
shoka, wala mapanga kama walivyo wenzetu, lakini kama ni mchaka mchaka
au karate tutapiga.
“Mtu yeyote
mwenye nia mbaya na nchi yake hawezi kutangaza hadharani, na sisi kwa
kuwa nia yetu ni njema na yenye lengo la kujilinda ndiyo maana
tulitangaza mchana kweupe,” alisema Mbowe.
Onyo kwa Tendwa
Kadhalika,
CHADEMA kimemwonya Msajili wa Vyama vya Siasa, John Tendwa, asijaribu
wala kuthubutu kukifuta chama hicho na kudai kuwa hatua hiyo
itasababisha maafa nchini.
Mbowe
alisema tamko la Tendwa linadhihirisha kile alichokiita ulevi wa
madaraka na kama angelikuwa chini ya uongozi makini alipaswa kufukuzwa
kazi mara moja kwa kauli zake zinazohatarisha demokrasia na amani ya
nchi.
“Kauli za
Tendwa zinazidi kuiponza serikali. Hazitawasaidia hata kidogo. Sasa
kauli ya Mbowe ambayo naomba imfikie Tendwa ni hii, ajaribu kufuta
CHADEMA aone moto wake.
“Unajua
anaposema atafuta CHADEMA, maana yake ni kwamba anafuta Kambi ya
Upinzani Bungeni, anafuta wabunge wote, hivyo uitishwe uchaguzi. Anafuta
madiwani 600 na zaidi nchi nzima, hivyo uchaguzi urudiwe; anafuta
wenyeviti wa vijiji, mitaa, vitongoji na wajumbe wao...huyu mtu amelewa
madaraka, ajaribu aone moto,” alisema Mbowe.
Upotoshaji wa amani
Mbowe
alisema kuwa kuna propaganda ambazo ama zinafanywa kwa makusudi au kwa
kutokujua, zikipotosha maana nzima ya amani ambayo kila Mtanzania hana
budi kuipigania.
Akimnukuu
Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere, kwenye moja ya hotuba yake aliyowahi
kuitoa mwaka 1986, Ukumbi wa Chuo cha Usimamizi wa Fedha (IFM), Dar es
Salaam, Mbowe alisema kama jamii haina wala haioni matumaini kwa
viongozi wao huku haki zikiminywa, amani haiwezi kudumu.
“Suala la
amani linafanyiwa upotoshaji mkubwa siku hizi. Ukisikiliza baadhi ya
redio siku hizi unasikia wamerekodi sauti sijui ya kiongozi au mtu
mashuhuri katika nchi, wanazungumzia amani, amani, amani, utafikiri
amani inapatikana kwa kuimbwa kama ngonjera. Amani ina misingi yake.
Misingi hiyo ikiwekwa au ikitekelezwa amani itadumu tu.
“Baba wa
Taifa Mwalimu Nyerere aliwahi kuhutubia akisema kuwa wakati anang’atuka
madarakani aliacha nchi ikiwa na amani, si kwa sababu watu hawakuwa
maskini, umaskini ulikuwepo, lakini kulikuwa na amani. Alisema ni kwa
sababu watu...wananchi walikuwa na amani na serikali yao. Walikuwa na
matumaini na viongozi wao, walikuwa wana amini katika Azimio la Arusha,
walikuwa wana matumaini ya haki katika nchi yao.
“Mwalimu
anasema wananchi walikuwa maskini, lakini walikuwa na matumaini kwa
sababu serikali yake ilikuwa imejenga usawa kwa binadamu, kulikuwa na
heshima kwa mkubwa na mdogo, mdogo na mkubwa. Ilikuwa imeweka misingi ya
haki na matumaini, ndiyo ilikuwa ikibeba na kulea amani yetu wakati
ule. Sasa vitu hivyo havipo.
“Wananchi
wakipoteza vitu hivyo, vikikosekana, amani inayodaiwa kuwepo inakuwa
sawa na volkano inayotikisika chini ya ardhi, inaweza kulipuka wakati
wowote. Sasa tunawaambia watawala wasiende majukwaani tu kuhubiri
amani...waweke miundombinu ya matumaini na haki kwa wananchi wote, bila
kujali dini zao, makabila yao, rangi zao, wala maeneo wanayotoka.
Alisema
wananchi wanahitaji kuona matumaini katika elimu yao, elimu ya watoto
wao, wananchi wanasumbuliwa na gharama za maisha zinazopanda kila
kukicha, tofauti za kipato zinazidi kuwa kubwa, wanataka wakienda
mahakamani watendewe haki, vinginevyo amani inayohubiriwa kwa maneno tu
bila miundombinu ya matumaini na haki, itakuwa ni amani ya muda mfupi
tu,” alisema Mbowe.
Katiba mpya
CHADEMA pia imeisuta CCM kwa kukataa masuala mengi ya msingi yaliyopendekezwa na Tume ya Jaji Joseph Warioba.
“Bahati
mbaya sana, mambo yote haya manne ambayo kwa kweli ni muhimu sana
yakawemo kwenye Katiba mpya ya Watanzania, CCM wanayapinga. Kwanza, kuna
suala la maadili na miiko ya viongozi, pili kuna suala la tunu za
taifa, tatu haki za binadamu na nne ni serikali tatu.
“Haya ni
kati ya mambo ya muhimu sana ambayo sisi CHADEMA tunaona ni vema
yakatajwa na kuzingatiwa kwenye Katiba mpya, lakini jamaa hawa (CCM)
hawayataki au mengine eti wanataka yasitajwe kwenye Katiba mpya bali
yaundiwe sheria.
“Yaani jamaa
hawa wanahofu, hawataki mambo ya tunu za taifa kama vile uwazi, ili
mikataba hii mibovu iliyopo kila mahali iwe mwisho, wanapinga hata haki
za binadamu, serikali tatu ndiyo balaa kabisa, wanajua wameondoka,”
alisema.
Aliongeza
kuwa chama hicho kitazunguka nchi nzima kuunda mabaraza yake ya katiba
ambayo siku nzima wananchi wa eneo husika watajadili rasimu ya Katiba
mpya wakitoa maoni yao.
No comments:
Post a Comment