EBENEZA MARCH 9 2014

EBENEZA MARCH 9 2014

Thursday, May 23, 2013

Gas City: Sospeter Muhongo Dodoma, wananchi wa Mtwara majumbani

Gas City: Sospeter Muhongo Dodoma, wananchi wa Mtwara majumbani


Wakati mjadala mkali ukitarajiwa kuibuka bungeni leo wakati Serikali itakapokuwa ikiwasilisha bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini, joto limezidi kupanda mkoani Mtwara ikielezwa kuwa wananchi wamehamasishana kwa mara nyingine kuacha shughuli zote ili kusikiliza kama hotuba hiyo italinda masilahi yao.
Waziri wa Nishati na Madini Profesa Sospeter Muhongo

Hotuba hiyo ambayo itasomwa leo mara baada ya kipindi cha maswali na majibu bungeni na Waziri wa wizara hiyo, Profesa Sospeter Muhongo, inatarajiwa kuibua mengi yakiwamo yanayohusu suala la gesi ya Mtwara.
Mjini Mtwara vipeperushi vinavyopingana vilisambazwa kuhamasishana ‘kuacha shughuli zao zote na kubaki nyumbani ili kufuatilia matangazo ya televisheni wakati
Profesa Muhongo atakapotangaza bajeti hiyo, huku vingine vikipinga.
Ahadi za matumaini
Licha ya kampeni hizo za watu wa Mtwara, Serikali nayo imeweka matangazo katika vyombo vya habari likiwemo gazeti hili ikieleza namna mikoa ya Mtwara na Lindi itakavyonufaika na utafutaji na uendelezaji wa Gesi Asilia.
Tangazo lililotolewa na Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania limeainisha faida za gesi hiyo kwa Mkoa wa Mtwara ukiwamo umeme utakaotokana na gesi asilia. Pia imeelezwa jinsi mafunzo kwa vijana juu ya matatizo ya gesi asilia yaliyodhaminiwa na Wizara ya Nishati na Madini na kampuni mbalimbali kuanzia mwaka 2010.
Vilevile imeelezwa jinsi uboreshaji wa huduma za jamii kama ujenzi wa shule, hospitali na ujenzi wa viwanda kama kile cha saruji cha Dangote na mitambo ya kusafishia gesi utakavyowanufaisha wakazi wa mkoa huo.
Gesi hiyo ambayo pia inachimbwa katika Kisiwa cha Songosongo inatajwa kwamba itawanufaisha wakazi wa Mkoa wa Lindi kwa kupata umeme, kunufaika na kodi ya wawekezaji wa gesi na udhamini wa mafunzo kutoka kampuni mbalimbali na wizara.
Wiki iliyopita Profesa Muhongo alijigamba kuwa bajeti ya wizara yake atakayosoma leo itakuwa ya karne ya 22 itakayomaliza tatizo la umeme nchini kwa kuwa imetoa vipaumbele kwa sekta binafsi kusaidia upatikanaji wa umeme wa uhakika.

Soma zaidi hapa

Mwalimu wa shule ya msingi kupandishwa kizimbani kwa kumjaza mimba mwanafunzi


Mwalimu wa shule ya msingi kata ya Msingi tarafa ya Kinampanda wilayani Mkalama Wolter Ponela mwenye umri wa miaka 32, anatarajiwa kupandishwa kizimbani katika mahakama ya wilaya ya Iramba kujibu tuhuma ya kumjaza mimba mwanafunzi wa kidato cha pili mwenye umri wa miaka 17.
Mwanafunzi huyo anasoma katika shule ya sekondari Jerumani iliyopo kata ya Msingi.
Mkuu wa wilaya ya Mkalama Edward Ole Lenga amesema kuwa, ofisi yake imesikitishwa na kitendo cha mwalimu huyo kwa madai kuwa kinachangia kuharibu maisha ya msichana husika.
Mkuu wa wilaya mpya ya Mkalama mkoani Singida, Edward Ole Lenga

Amesema kuwa, vitendo hivyo ni lazima vipigwe vita na wadau wote wa elimu ili kuhakikisha wanafunzi wa kike wanasoma hadi upeo wao bila vikwanzo.
Katika hatua nyingine, mkuu huyo wa wilaya amekemea vikali tabia iliyoota mizizi ya kumaliza kienyeji matatizo ya wanafunzi kubebeshwa mimba.
Lenga amesema kuwa, ni lazima sheria zilizowekwa zitumike katika kukomesha tabia za kuwajaza mimba wanafunzi ambazo huwa hazitarajiwi au mimba za utotoni.
Aidha, ameagiza watendaji  kila mmoja katika maeneo yake aorodheshe majina ya wanafunzi waliojazwa mimba na watu waliochangia uharibifu huo wa mimba za utotoni.
Aidha, Lenga amewataka walimu kutenga muda kuwaelimisha wanafunzi wa kike madhara yatokanayo na mimba za utotoni kama njia moja wapo itakayosaidia wanafunzi kuchukia vitendo vya mahusiano ya kimapenzi wakati wakiwa shuleni.

No comments:

Post a Comment