EBENEZA MARCH 9 2014

EBENEZA MARCH 9 2014

Thursday, February 13, 2014

Msigwa : kikwete aficha ikweli kuhusu ujangili wa tanzania

Waziri Kivuli wa Maliasili na Utalii, Mchungaji Peter Msigwa.PICHA|MAKTABA 


Dar es Salaam. Waziri Kivuli wa Maliasili na Utalii, Mchungaji Peter Msigwa, ameitaka Serikali kutoa majibu sahihi baada ya gazeti la Daily Mail on Sunday la Uingereza, kuchapisha habari inayoeleza kuwa Tanzania ni kinara wa ujangili, huku Rais Jakaya Kikwete akifumbia macho.
Akizungumza na waandishi wa habari jana, Mchungaji Msigwa alisema maelezo yaliyotolewa na Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu baada ya kuchapishwa kwa taarifa hizo yamejaa siasa, uzushi na uongo.
Alisema ukweli lazima uwekwe wazi kwa sababu wanaohusika na biashara hiyo ni baadhi ya watendaji wa Serikali, wafanyabiashara na vigogo wa vikosi vya ulinzi na usalama nchini.
Wakati Mchungaji Msigwa akieleza hayo, Ikulu ya Marekani jana ilitoa taarifa ya kupiga marufuku biashara ya meno ya tembo nchini humo ikiwa ni hatua yake ya kukabiliana na ujangili ulioshika kasi katika nchi za Afrika, ikiwemo Tanzania.
Pia, leo Rais Kikwete atakuwa miongoni mwa viongozi 50 watakaohudhuria mkutano wa kuokoa viumbe vilivyo hatarini kutoweka duniani, unaofanyika London, Uingereza.
Mkutano huo utakuwa chini ya wenyeji wa mwana wa Wales na Waziri wa Mkuu wa Uingereza, David Cameron.

Taarifa ya gazeti hilo ya Februari 8 mwaka huu, limeitaja Tanzania kama kinara wa ujangili kwa kuua zaidi ya tembo 11,000 kwa mwaka na kumhusisha Rais Kikwete kuwa na urafiki na wafanyabiashara ya meno ya tembo.
Pia imewahusisha wafadhili wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), katika biashara hiyo.
Katika maelezo yake Mchungaji Msigwa alisema, “Takwimu za Serikali zinaeleza wazi mwaka 2010 tembo 10,000 waliuawa nchini sawa na wastani wa tembo 37 kwa siku. Inakuwaje taarifa hizi ziwekwe wazi halafu Serikali idai inachafuliwa.”
Alisema Serikali imewahi kukiri kuwa inawajua wanaojihusisha na ujangili lakini badala ya kuwakamata imekuwa ikiwataka kuachana na biashara hiyo.
“Inakuwaje mtu anayevunja sheria za nchi hakamatwi. Waziri Nyalandu amekuwa mlalamikaji badala ya kutafuta suluhu, majibu yake na ya Serikali ya CCM yanadhihirisha kuwa mtandao huu unaogopwa unaihusisha Ikulu, wanasiasa, polisi, maofisa wanyamapori na wanajeshi,” alisema.
Msigwa alisema ni jambo la kushangaza kuona kuwa hadi sasa Serikali haijawakamata watu wanaouza meno ya tembo ambao wameonekana katika makala ya uchunguzi iliyorushwa na Kituo cha Televisheni cha ITV cha Uingereza.
>>Mwananchi

No comments:

Post a Comment