Waziri wa Nchi ofisi ya Rais (Mahusiano na Uratibu) Stephen Wassira
akizungumza na waandishi wa habari baada ya kuhojiwa na kamati ya
maadili ya CCM mjini Dodoma .
na Mpigapicha wetu
Posted Februari15 2014 saa 9:0 AM
Dodoma. Kamati ndogo ya Maadili ya CCM
imeendelea kuwahoji wanachama wake walioonyesha nia ya kuwania urais,
jana ilikuwa zamu ya mawaziri watatu.
Waliohojiwa jana ni Waziri wa Mambo ya Nje na
Ushirikiano wa Kimataifa, Benard Membe, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais
Mahusiano na Uratibu, Stephen Wassira na Naibu Waziri wa Mawasiliano,
Sayansi na Teknolojia, Januari Makamba. Makamba alikuwa wa kwanza kufika
mbele ya kamati hiyo jana asubuhi, huku Wassira akifuatia. Hata hivyo,
Membe hakuonekana.
Hata hivyo, kanuni za uongozi wa maadili za CCM
kifungu cha 7 (i) kinaeleza kuwa wanachama wenye nia ya kugombea nafasi
za uongozi katika muhula unaofuata, yaani ubunge, uwakilishi, udiwani na
nafasi nyingine katika chama wanaweza kutangaza nia zao, lakini
hawaruhusiwi kufanya kampeni kabla ya muda uliowekwa rasmi, muda wa
kampeni unaanza baada ya majina ya wagombea kuteuliwa na kikao
kinachohusika.
Makamba
Baada ya kuhojiwa Makamba, alisema siyo vibaya kwa
wanaotaka kuwania urais katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015 kutangaza
nia mapema, kwa sababu inawapa nafasi wananchi kuwapima.
Mbali na hilo Makamba alisema siyo dhambi kwa mtu
kuonyesha nia, bali ni dhambi kwa mtu kutoa fedha kwa nia ya kutaka
uongozi na kuvitaka vyombo vya dola kuchukua hatua za kisheria kwa watu
wa aina hiyo.
Kikao hicho kinachoongozwa na Makamu Mwenyekiti
Bara, Philip Mangula, juzi kiliwahoji mawaziri wakuu wa zamani Edward
Lowassa na Fredrick Sumaye pamoja na Mbunge wa Sengerema, William
Ngeleja, ambaye pia aliwahi kuwa Waziri wa Nishati na Madini.
“Ipo faida ya kuwajua mapema wanaotaka uongozi
kuliko kuwajua mwishoni, kwa sababu mnapata faida ya kuwachambua na
kuwauliza maswali, mbaya ni mtu kutoa pesa ama kutumia pesa.
“Hata katika maoni yangu na ushauri (ndani ya
kikao hicho cha maadili), nimesema kwamba hilo ndilo kubwa na la msingi,
kwa sababu linawaweka pembeni watu wenye vipaji vya uongozi kama huna
fedha basi huwezi kuwa kiongozi,” alisema Makamba.
Alisisitiza matumizi ya fedha katika kutafuta
uongozi yanakatazwa kwa mujibu wa kanuni za chama chao na sheria za nchi
na kwamba ushahidi unapopatikana chama kifanye kazi yake na Serikali
ichukue hatua dhidi yao.
Makamba alisema ipo sheria ya Taasisi ya Kuzuia na
Kupambana na Rushwa (Takukuru) na Sheria ya Gharama za Uchaguzi, ambazo
zote zinakataza matumizi ya fedha.
“Kwa hiyo hawa wanaotajwa wanatumia fedha vilevile yombo vya dola viwachukulie hatua, siyo tu kwenye chama,” alisema Makamba.>>>Mwananchi
No comments:
Post a Comment