kamanda wa polisi mkoa wa Arusha Leberatus sabasi |
Jeshi la Polisi Mkoani hapa limemkamata mwanamke mmoja
aitwaye Imelda Juma (20) Mkazi wa Sokoni One jiji hapa akiwa na noti bandia
zenye thamani ya Tsh 6,140,000 (Milioni sita laki moja na elfu orobaini).
Akizungumza na SWACOTZ fisini kwake, Kamanda wa Polisi Mkoa
wa Arusha Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Liberatus Sabas alisema
kwamba tukio hilo lilitokea tarehe 13.12.2013 muda wa saa 10:00 Alasiri katika
maeneo ya Kituo kikuu cha Mabasi mara baada ya jeshi hilo kupata taarifa toka
kwa raia wema.
Kamanda Sabas alifafanua kwa kusema kwamba, siku ya tukio
mtuhumiwa ambaye ni Imelda Juma alimtuma dereva wa pikipiki maarufu kama “boda
boda” aitwaye Jamal Abdul ili aende maeneo ya Sakina Darajani kwenda kuchukua
mzigo. Mara baada ya dereva huyo kufika katika eneo hilo aliukuta mzigo huo
ukiwa pembeni ya pikipiki nyingine ambayo haikuwa na mtu.
Dereva huyo wa pikipiki aliuchukua mzigo huo na kuupeleka
katika kituo cha mabasi cha Dar Express kama alivyoelekezwa na mtuhumiwa ambaye
ndio mmiliki wa mzigo huo ili autume kwa mtu aliyefahamika kwa jina moja la
Emmanuel ambaye inadaiwa yupo Dar es salaam.
Wafanyakazi wa kampuni ya mabasi ya Dar Express waliokuwa
ofisini hapo hawakuwa tayari kuupokea na kuusafirisha mzigo huo bila kuufungua
ili wajiridhishe japokuwa dereva wa boda boda alikataa kufungua mzigo huo kwa
madai kwamba mwenye mzigo alimwambia hasikubali mzigo huo ufunguliwe.
“Ndipo wafanyakakazi hao wakamshauri dereva huyo wa boda boda
kama hataki ufunguliwe basi naye pia akate tiketi ili asafiri pamoja na mzigo
wake mpaka Dar es salaam”. Alisema Kamanda Sabas.
Mara baada ya taarifa hiyo kufika katika kituo kikuu cha
Polisi, askari waliweka mtego na kumkamata mtuhumiwa huyo Imelda Juma ambaye
inasemekana alikuwa maeneo ya karibu na hapo.
Mpaka hivi sasa Jeshi hilo linaendelea kumhoji mtuhumiwa huyo
ili kuweza kubaini mtambo unaotengeneza fedha hizo bandia huku pia likiendelea
kumtafuta mtumiwa mwingine aitwaye Emmanuel.
Kufuatia tukio hilo Kamanda Sabas ameendelea kuwashukuru
wananchi wa Mkoa huu kwa jinsi wanavyoshirikiana na jeshi hilo juu ya utoaji wa
taarifa kwani fedha hizo kama zingesambaa mtaani kwa ajili ya matumizi
zingedhoofisha uchumi wa nchi kwa kiasi fulani.
Aidha amewatahadhalisha wananchi wa Mkoa huu hasa
wafanyabiashara kuwa makini na noti mbalimbali wanazozipokea toka kwa wateja
wao, kwani wengine hutumia mwanya wa wingi wa noti kupenyeza fedha bandia.
$
No comments:
Post a Comment