SERIKALI ya Uingereza inatafakari ombi
la Tanzania la mabehewa na injini za treni, ambayo nchi hiyo haizitumii
tena, lakini bado ni nzima kwa ajili ya kusaidia kuimarisha usafiri wa
reli katika Tanzania na hasa wa Jiji la Dar es Salaam.
Ahadi hiyo ya Uingereza ilitolewa na
Naibu Waziri Mkuu wa Uingereza, Nick Clegg wakati wa mazungumzo yake na
Rais Jakaya Kikwete kwenye hoteli ya Sheraton, Davos, Uswisi, ambako
viongozi hao wawili walikuwa wanahudhuria Mkutano wa Taasisi ya Uchumi
Duniani (WEF) mwaka huu.
Katika mazungumzo yao katikati ya wiki
hii, Rais Kikwete alizungumzia hatua za Serikali ya Tanzania za
kuimarisha usafiri hasa ule wa reli mjini Dar es Salaam na ile ya kwenda
Bara.
Katika mazungumzo hayo ambayo
yalihudhuriwa pia na Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Christopher
Chiza na Waziri wa Uchukuzi, Dk Harrison Mwakyembe, Rais alimwomba Clegg
kuangalia uwezekano wa nchi hiyo kutoa mabehewa na injini ambazo
hazitumiki tena Uingereza ambako Rais alisema kuwa bila shaka bado
zinafaa kwa Tanzania.
Akielezea hali ya usafirishaji wa mizigo
kwa njia ya reli nchini, Waziri Mwakyembe alisema kutokana na uchakavu
wa reli na ukosefu wa injini na mabehewa ya kutosha ni kiasi cha tani
300,000 tu za mizigo zinazosafirishwa kwa reli kati ya mizigo tani
milioni 13.7 ambayo inasafirishwa nchini kila mwaka.
Alisema kuwa kiasi kilichobakia
kinasafirishwa kwa barabara. “Mheshimiwa unaweza uzito wa ninayoyasema
kwa sababu tunajenga barabara nyingi nchini, kila kona, lakini
usafirishaji wa namna hii wa mizigo kwa barabara utaharibu kabisa
barabara hizo katika muda mfupi,” Rais Kikwete alimwambia Clegg.
Katika mazungumzo hayo, Rais Kikwete
aliishukuru Serikali ya Uingereza kwa kuendelea kuunga mkono maendeleo
ya Tanzania kwa kusaidia nyanja za elimu, afya na maji na pia kuendelea
kuwa nchi inayoongoza duniani kwa makampuni yake kuwekeza katika uchumi
wa Tanzania. Rais pia alimwomba Clegg kusaidia kuvutia uwekezaji zaidi
kutoka Uingereza kuja Tanzania kwa kuisemea vizuri Tanzania.
“Neno lako moja la kusifia Tanzania lina
nguvu zaidi kuliko hotuba zangu kwa makampuni na wenye makampuni katika
Uingereza.” Viongozi hao pia walizungumzia umuhimu wa kukamilisha
Mikataba ya Ushirikiano wa Uchumi ya EPA kati ya nchi za Afrika na nchi
za Ulaya.
Walikubaliana kuwa mjadala wa jambo hilo
umechukua muda mrefu kupita kiasi na sasa ni wakati wa kufikia mwisho
wa jambo hilo. Rais Kikwete alimwambia Naibu Waziri Mkuu huyo kuwa moja
ya masharti ambalo yanayoikwaza Afrika katika kufikia makubaliano ya
mikataba hiyo ni lile la kuzilazimisha nchi za Afrika kufungua masoko
yao kwa namna ile ile ya yatakavyofunguliwa masoko ya nchi za Ulaya.
“Hofu yetu hasa ni kuhusu jambo hilo. Ni
vigumu, kwa mfano, kwa makampuni ya ujenzi ya Tanzania kushindania
tenda moja na kwa masharti yale yale na makampuni ya Uingereza kwa
sababu wakati mwingine unaweza kufungua uwanja ukawa sawa lakini
wachezaji wasiwe na uwezo unaofanana.”
Wakati wa mazungumzo hayo, Rais Kikwete
alimkaribisha Clegg kutembelea Tanzania, ombi ambalo Naibu Waziri Mkuu
alilikubali kimsingi akisema kuwa anatamani sana kuja tena Tanzania kwa
sababu miaka 13 iliyopita aliitembelea Tanzania kwa mapumziko na mkewe
baada ya kuwa wamefunga ndoa.
HABARI LEO
No comments:
Post a Comment