Mmoja
wa viongozi wake ametoa taarifa iliyojaa maneno makali akimshambulia Lowassa na
baadhi ya viongozi wa dini akiwahusisha na kampeni za uchaguzi wa urais
mwakani.
Bila
kutaja jina la kiongozi yeyote wa dini, ila tu kurejea kwa ujumla wao kama
maaskofu na masheikh, Katibu wa Uhamasishaji na Chipukizi wa UVCCM, Paul
Makonda, aliwataka kwenda kwa Lowassa kama wanataka fedha za haraka. Hakusema
ni fedha za nini.
Akizungumza
katika mkutano wa waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Makonda
alisema hawawezi kukaa kimya wakati viongozi wa CCM wakishambuliwa na watu
aliosema hawana mapenzi mema na chama chao.
Alisema
wapo watu aliodai wanafadhiliwa na Lowassa ili kuwashambuliwa viongozi wa
sekretariati ya CCM, Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana na Katibu wa
Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, kwa kuwa anautaka urais mwakani.
Aliwataja
makada wa CCM aliodai wanaosukumwa na Lowassa kuwa ni Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa
Singida, Mgana Msindai na Mwenyekiti mstaafu wa CCM Dar es Salaam, John
Guninita.
Makonda
aliwatuhumu makada hao kuwa ni wahaini, waongo na wazandiki, na kueleza kuwa
kama nia yao ni kusaka urais kwa ajili ya Lowassa, basi wajue kuwa amekosa sifa
za kuteuliwa na chama hicho kuwania wadhifa huo katika uchaguzi mkuu wa
mwakani.
Hata
hivyo, muda mfupi tu baada ya kauli ya Makonda, Makamu Mwenyekiti wa UVCCM,
Mboni Mhita, alisema kauli hiyo siyo msimamo wa UVCCM.
Msindai
alikaririwa hivi karibuni akielezea msimamo wa kumuunga mkono Lowassa katika
masuala ya maendeleo, wakati Guninita alimkosoa Katibu wa Itikadi na Uenezi,
Nape Nnauye, kutokana na kauli zake za kuwaita baadhi ya mawazi ‘mizigo’ kwa
kuwa wameshindwa kutekeleza ilani ya CCM ya mwaka 2010-2015.
Pia
alimlaumu Nape kwa kukosoa uteuzi mpya wa baraza la mawaziri uliofanywa na Rais
Jakaya Kikwete Januari 19, mwaka huu.
Guninita
alimkosoa Nape akisema kuhoji uteuzi huo ni sawa na kuingilia mamlaka ya Rais
katika kutimiza wajibu wake kwa kikatiba.
Katika
mkutano na waandishi wa habari jana Makonda alisema: “Tutaendelea kuwajibu
akina Msindai (Mgana) ama Guninita (John), lakini kuna mtu anayewatuma kutoa
kauli hizo, na huyu ni Edward Lowassa.”
NIPASHE
iliwasiliana na Lowassa kwa njia ya simu jana, lakini ikapokewa na mtu
aliyeagiza suala hilo aulizwe mmoja wa wasaidizi wake wa masuala ya vyombo vya
habari.
Msaidizi
huyo ambaye hakutaka jina lake litajwe gazetini, alisema Lowassa hawezi
kuzungumzia madai ya Makonda.
Makonda
alisema UVCCM imemuandikia barua Makamu Mwenyekiti wa CCM Bara, Philip Mangula,
kuhusu vitendo vya Lowassa kuwatumia viongozi na makada wa chama hicho kutoa
kauli zenye mwelekeo wa kumchonganisha Rais Kikwete na sekretarieti ya chama
hicho.
Alisema
barua hiyo (hakuionyesha) ililenga kumuomba Mangula, asaidie ili kanuni za
chama hicho zitumike kumdhibiti Lowassa.
NIPASHE
ilimtafuta Mwenyekiti wa UVCCM, Sadifa Hamisi Juma, kuzungumzia kauli ya
Makonda kama ndiyo msimamo wa jumuiya hiyo, lakini simu yake haikujibiwa wala
ujumbe mfupi wa maneno (sms) hadi tunakwenda mitamboni jana
Akifafanua
kauli hiyo Mhita alisema ni ya Makonda kama mkuu wa kitengo cha uhamasishaji.
“Kama
utafika wakati ikahitajika kuzungumzia jambo lolote la kitaifa, basi
mzungumzaji mkuu ni Mwenyekiti wa UVCCM au Makamu Mwenyekiti,” alisema Mhita
pasipo kufafanua zaidi.
NIPASHE
ilipowasiliana na Msindai na Mangula, simu zao ziliita bila kupokelewa wakati
ile ya Guninita haikupatikana.
Awali,
Makonda alisema ziara ya Kinana na Nape (iliyowaibua mawaziri mizigo) ilikuwa
sehemu ya utekelezaji wa kanuni, misingi na katiba ya CCM, vinavyotoa jukumu
kwa chama hicho kuwa kiungo kati ya serikali na wananchi.
Alisema
CCM ni chama kinachoiunganisha serikali na wananchi, na kwamba ziara ya Kinana
iliyokuwa na wajumbe kadhaa akiwamo Nape, ilifanikisha kuibua kero kadhaa
zilizopo kwenye jamii.
Makonda
alisema kupitia ziara hiyo, ujumbe wa Kinana ulibaini kuwapo kero
zilizowasilishwa serikalini kwa nia ya kupatiwa ufumbuzi, hivyo inashangaza
kuibuka kwa baadhi ya wana-CCM wanaoikejeli.
Kwa
mujibu wa Makonda, ziara kama iliyofanywa na Kinana, haijawahi kufanywa na
kiongozi yeyote wa ngazi hiyo kwa miaka ya karibuni, na kusema wanaoipinga
hawana nia njema na wananchi wanaokabiliwa na kero mbalimbali za kijamii.
“Chama
hiki ni cha wanyonge, maskini wa taifa hili, haiwezekani matajiri watake
kukihodhi na waratibu mikakati ya kukihujumu kwa fedha, hali sisi vijana
tukitazama, tunasema tutakilinda na tutawalinda viongozi wetu waadilifu,”
alisema.
Makonda
alisema viongozi wanaobezwa (Kinana na Nape) wamechangia kurudisha imani ya
wananchi kwa CCM, akitoa mfano wa kukutana na `kuzichukua’ kero za wafugaji,
walimu, wakulima wa pamba, korosho na wananchi wa kawaida.
UVCCM
RORYA YAMVAA MAKONDA
Katika
hatua nyingine, Mwenyekiti wa UVCCM Wilaya ya Rorya, Sango Kasera, amemtaka
Katibu Mkuu wa Umoja huo, Sixtus Mapunda, kueleza kama tamko lililtolewa na
Makonda ni la kamati ya utekelezaji au ni lake binafsi.
Pamoja
na kumtaka Mapunda kueleza hilo, pia amemtaka Makonda kufanya kazi za kufufua
chipukizi na kueleza kazi walizofanya kama UVCCM hadi sasa, kwani tangu
ateuliwe amekuwa akiishia tu kutoa matamko, ambayo hayana tija kwa vijana wa
Kitanzania.
CHANZO:
NIPASHE
No comments:
Post a Comment