EBENEZA MARCH 9 2014

EBENEZA MARCH 9 2014

Saturday, March 22, 2014

KAULI YKE MWENYEWE MOURINHO AKUBALI KUINOA MAN U BADALA YA DAVID MOYES

Kocha wa Man United, David Moyes (kushoto) na Jose Mourinho (kulia).
LONDON, England
MARA baada ya Kocha Sir Alex Ferguson wa Manchester United kutangaza kuwa atastaafu kufundisha soka, majina mengi ya makocha watakaochukua nafasi yake yalitajwa. Jose Mourinho ambaye kipindi hicho alikuwa akiinoa Real Madrid, alikuwa mmoja wa waliotajwa kwa wingi.

Bahati haikuwa yake, Kocha David Moyes aliyekuwa Everton akapata nafasi hiyo, wengi hawakutegemea, lakini inavyoonekana Mourinho aliumia, kwani inaaminika ana mapenzi na Man United na bado anatamani kuifundisha timu hiyo licha ya kuwa sasa ni bosi wa Chelsea.

Kutokana na mwenendo mbaya wa United kipindi hiki, baadhi ya wachambuzi wa soka wanaamini kuna uwezekano mkubwa wa kocha huyo kukubali kuifundisha United hata leo hii endapo itatokea United imemtimua Moyes, kisha yeye akahitajika kutua klabuni hapo.

Zifuatazo ni sababu chache zinazoonyesha kocha huyo raia wa Ureno ana mapenzi na timu hiyo maarufu kwa jina la Mashetani Wekundu licha ya kuwa anaiongoza vema Chelsea:

Kuonyesha heshima anapokutana nayo
Achana na ile mara ya kwanza alipokuwa Porto, tangu Mourinho alipoondoka England mara ya kwanza, amekuwa akiizungumza vizuri United na kuonyesha heshima kubwa kwa Ferguson tofauti na makocha wengine.

Wakati alipokuwa Madrid, siku timu yake ilipocheza dhidi ya United, Mourinho alionekana kuwa mwenye nidhamu kubwa tofauti na awapo uwanjani wakati timu yake ikicheza dhidi ya timu nyingine.

Hata mara baada ya mechi hiyo ambayo Madrid ilishinda, alisema: "Timu bora imepoteza mchezo.”

Kumtetea Alex Ferguson
Wakati Ferguson alipomweka benchi straika wake tegemeo, Wayne Rooney, katika Ligi ya Mabingwa Ulaya msimu uliopita, Mourinho alisema: "Sir Alex ameshinda kwa kufanya maamuzi mengi magumu, kila anachofanya yupo sawa na haihitaji maswali, ni kocha aliyetengeneza historia."

Kuitetea United ilipoyumba
Mwanzoni mwa msimu huu, United ilikuwa ikiyumba kama ilivyo sasa, haikupata matokeo mazuri, lakini Mourinho alipoulizwa alisema: “United ni United, inaweza kufanya lolote na muda wowote.”


United bado ni timu kubwa
Mourinho yupo Chelsea, ni timu kubwa lakini kwa sifa na rekodi za ubora bado haijafikia kuwa daraja moja sawa na AC Milan, Barcelona, Liverpool, Real Madrid, Juventus na Inter Milan, hivyo nafasi hiyo ni kubwa.

Heshima kila anapocheza dhidi ya United
Mara kadhaa imewashangaza wengi kuwa Mourinho anapocheza dhidi ya timu kubwa nyingine ni jambo la kawaida kukwaruzana na wapinzani, iwe wachezaji au makocha, lakini anapofika Old Trafford huwa anaonyesha heshima na kuwa mstaarabu.

Hana maneno ya ‘shombo’ akikutana na Mashetani hao, lakini mara nyingi amekwaruzana na mabosi wa timu nyingine kama vile Manchester City na Arsenal.
 
Kujulishwa na Ferguson kinachoendelea
Hivi karibuni Mourinho alisema mara baada ya United kufanya maamuzi ya kumchukua Moyes, alipata taarifa hizo mapema kutoka kwa Ferguson mwenyewe, wengi wanajiuliza kwa nini kocha huyo mkongwe alienda kumjulisha! Wanaamini kuna ukaribu zaidi ya urafiki juu ya taarifa hizo.

Katika kura za maoni zilizopigwa kwenye mitandao barani Ulaya zinaonyesha kuwa mashabiki wengi wa United wamekubali hoja kuwa United ingemchagua Mourinho kuliko Moyes.
Kura hizo zipo hizi
Wanaomtaka Mourinho 80.9%
Wasiomtaka Mourinho 19.1%
Jumla ya kura: 8,114
Wewe shabiki wa Tanzania unadhani Mourinho alikuwa ni mtu sahihi kuinoa United? Tuma maoni katika namba 0719 137090. Maoni yako yatachapishwa Ijumaa ijayo katika gazeti hili.

No comments:

Post a Comment